Uzalishaji kapunga wapanda ,aksante kwa teknolojia mpya

MBARALI 8.7.2018

MATUMIZI ya teknolojia za kisasa kumewezesha uzalishaji katika mradi wa Kapunga kuongezeka na kufikia wastani wa asilimia 6.5 ya uzalishaji kwa hekta moja.

Kauli hiyo imetolewa na Ofisa rasilimali watu wa Kampuni ya Kapunga, Fatma Ally wakati akielezea maendeleo ya mradi huo kwa waandishi wa habari mwishoni mwa wiki.

Alisema kitakwimu hali ya uzalishaji wa mpunga imeongezeka kutoka tani 20,000 mpaka 22,000 kwa mwaka 2016/18 na kwamba kiwanda hicho kina uwezo wa kusafisha,kukoboana kufungasha tani 100 za mchele kwa siku.

Fatma alisema kuwa wamekuwa wakishirikiana wakulima 350 katika kilimo kwa makubaliano maalum hususan kuwapatia mafunzo ,kuwaandalia mashamba ,mbolea na kisha kuwavunia jambo linalowapatia mafanikio makubwa ya upatikanaji wa mazao.

Naye Mwenyekiti wa Kikundi cha wakulima Wanawake wanaojihusisha na kilimo cha zao Mpunga Stumai Willison kupitia Kampuni ya Kapunga wameipongeza kampuni hiyo kwa kuwajengea uwezo wa kuzalsiha zao hilo kwa wingi.

Alisema kuwa awali walikuwa wakilima zao hilo kwa mazoea jambo lilikuwa likisababisha kupata mazao kidogo na baada ya kupata elimu, shamba,pembejeo za kilimo na mbegu kutoka kapunga wameweza kuzalisha mpunga gunia 218 katika msimu huu wa kilimo.

Aidha alisema mbali na mafanikio hayo pia wanaomba wapatiwe eneo kubwa kwa ajili ya uzalishaji wa mpunga ili kuunga mkono jitihada za Serikali za uchumi wa viwanda.

Katibu wa kikundi Salome Magida alisema mbali na kuwepo kwa mahitaji ya maeneo kwa ajili ya kilimo wameweza kunufaika kupitia uwekezaji uliopo katika kijiji hicho katika nyanja za elimu, afya, miundombinu ya barabara na maji .

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Mbarali, Kivuma Msangi aliwashauri wakulima kujiunga katika vikundi ili kuweza kunufaika na mikopo ya asilimia 10 ya wanawake,vijana na walemavu.

Msangi alisema kuwa kwa mwaka 2017/18 wamefikia asilimia 95 ya utoaji wa mikopo , ambapo asilimia 4 zimetolewa kwa wanawake,na silimia 4 kwa wanaume na walemavu asilimia2.

Wakati huo huo wakazi wa kijiji cha Kapunga wilayani Mbarali Mkoani Mbeya wametakiwa kuepuka migogoro na mwekezaji wa Kampuni ya Kapunga Rice Project Limited ili waweze kunufaika na miradi mbalimbali ya maendeleo.

Kauli hiyo imetolewa na Makamu wa Rais, Samia Suluhu mwishoni mwa wiki wakati akizungumza na wananchi katika Mkutano wa hadhara uliofanyika Kijiji cha Kapunga kata ya Itamboleo Wilayani Mbarali Mkoani Mbeya mara baada ya kukagua kituo cha afya kilichojengwa na Kampuni ya Kapunga na mashine za kisasa za kukoboa mpunga .

Alisema Uwekezaji katika Mradi wa Kapunga umekuwa ni chachu kubwa kwa wananchi wanaozunguka mradi huo na kwamba ni wakati sasa kujenga uhusiano mazuri ili kuweza kunufaika zaidi.